UTENZI WA AL-INKISHAFI: DHIHIRISHO LA UHALISIAJABU KATIKA KUENDELEZA MAUDHUI YA DINI YA KIISLAMU
Abstract
Utafiti huu unahusu uchanganuzi wa kihalisiajabu kuendeleza maudhui ya dini katika Utenzi wa Al-Inkishafi wa Sayyid Abdallah bin Ali bin Nassir, mshairi mtajika aliyeishi katika kisiwa cha Pate baina ya 1718-1815 (Chiraghdin, 1987). Utenzi wa Al-Inkishafi ni mojawapo ya tungo tatu za kale maarufu sana Uswahilini hasa maeneo ya pwani Kaskazini. Utafiti huu umeangazia matumizi ya uhalisiajabu katika Utenzi wa Al-Inkishafi kuendeleza maudhui yanayoibua falsafa ya kidini kuhusu maisha ya binadamu. Vipengee vya kihalisiajabu katika kiwango cha wahusika na mandhari vimebainishwa na kuchanganuliwa katika mizani ya maisha ya jumuia ya Pate na mapisi yake ili kuendeleza maudhui ya dini. Uajabu wa wahusika na mandhari ulikuwa kichocheo msingi kwa mtafiti kuamua kushughulikia mada hii. Uchanganuzi huu uliongozwa na nadharia ya uhalisiajabu iliyoasisiwa na Franz Roh mwaka wa 1925 ambayo inayatazama matukio katika maisha ya binadamu kwa upeo ulio juu ya uhalisia kama ulivyozoeleka au kufahamika na binadamu; huangazia ulimwengu wa kidhahania sio ukweli kama ulivyo katika mazingira. Uteuzi wa sampuli ni Utenzi wa Al-Inkishafi wa Sayyid Abdallah bin Ali bin Nassir. Malengo ya utafiti huu yamekuwa: kubainisha wahusika na mandhari yanayodhihirisha uhalisiajabu, kueleza namna wahusika na mandhari ya uhalisiajabu yanavyoendeleza maudhui na kubainisha athari za maudhui ya dini kwa waumini zinazosawiriwa katika Utenzi wa Al-Inkishafi. Data ya kimsingi ilikusanywa maktabani kwa kusoma kazi teule, vitabu, majarida, tasnifu na katika mtandao. Data iliyopatikana ilichanganuliwa kwa kuzingatia malengo ya utafiti na nadharia teule. Aidha, mifano iliyotumika imetoka katika Utenzi wa Al-Inkishafi kulingana na ufanifu wake. Utafiti huu umeweka bayana kwamba uhalisiajabu kama mkabala wa kifasihi unadhihirika katika Utenzi wa Al-Inkishafi (1810-1820) kuendeleza
vi
maudhui ya dini japo uliasisiwa mwaka wa 1925 zaidi ya miaka mia mbili baada ya kutungwa utenzi huu.

